Vijiji 25 kunufaika biashara ya kaboni Arusha

Mkuu wa Wilaya ya Longido Marko Ng'umbi (kushoto) akikabidhi cheki ya zaidi ya Sh 372.3 milioni kwa vijiji vitano, fedha iliyotolewa na kampuni ya Soil for the Future Tanzania kwa ajili ya utekelezaji wa mradi wa uvunaji wa hewa ya Kaboni kwenye udongo kwa nyanda za malisho.  Picha na Bertha Ismail

Muktasari:

  • Vijiji vitano mkoani Arusha vimetia saini makubaliano na kampuni ya Soils for the Future (Tanzania) Ltd ya kutekeleza mradi wa uvunaji kaboni kwenye eneo la hekta 71,656.30, ambayo ni maeneo ya malisho.

Arusha. Wananchi katika vijiji 16 vilivyopo Wilaya ya Longido na Monduli (9) mkoani Arusha wanatarajiwa kupata Sh33 bilioni kila mwaka kupitia utekelezaji wa mradi wa uvunaji kaboni.

Mradi huo unahusisha kudumisha hatua za uhifadhi wa hekta milioni 2.4 utazalisha tani milioni 1.9 za hewa ya Kaboni zenye thamani ya Dola za Marekani 12.7 milioni, sawa na Sh33 bilioni.

Hayo yamebainika Juni 20, 2024 wakati wa makabidhiano ya fedha za awali, zaidi ya Sh372 milioni kwa vijiji vitano vilivyoanza utekelezaji wa mradi huo baada ya kusaini mkataba na Kampuni ya Soils for Future Tanzania Limited.

Vijiji vinavyoanza kufaidika ni Kimokuwa, Ngoswak, Sinonik, Loondolwo na Noondoto.

Vijiji vina jukumu la kupanga matumizi sahihi ya ardhi, ulinzi wa mazingira na utekelezaji wa programu zingine za mitaa.

Akikabidhi hundi hiyo yenye thamani ya Sh372.33 milioni, Mkuu wa Wilaya ya Longido, Marco Ng’umbi ameipongeza kampuni ya Soils for the Future Tanzania kwa kupeleka miradi hiyo kwa walengwa.

"Hii itahimiza jamii kuja na mipango sahihi ya matumizi ya ardhi, kuweka ardhi ya kutosha kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira pamoja na maeneo ya malisho," amesema.

Amesema maeneo mengi yaliyojitolea kwa biashara ya kaboni ni ya malisho, ambayo yana majukumu mawili, biashara ya kaboni na malisho.

"Itasaidia katika shughuli za kiuchumi za ufugaji kama tegemeo kubwa la wakazi wa wilaya hii, kupitia nyanda za malisho ambazo sasa ni ya uvunaji kaboni na kuvipatia vijiji fedha,” amesema.

Zaidi ya hayo, amesema Sh372.33 milioni zitatumika kwa mabadiliko ya malisho na kuanza utekelezaji mradi wa kaboni.

"Vijiji hivyo vitano vimefuzu kwa mradi wa kaboni baada ya kutia saini mkataba wa makubaliano na kuandaa na kuwasilisha mapendekezo ya jinsi ya kutumia pesa zilizopatikana," amesema mratibu wa mradi wa kaboni wa kampuni hiyo, Richard Ndaskoi.

Ndaskoi amesema mradi wa kaboni, utakaotekelezwa kwa miaka 40, utahusisha hekta milioni 2.4 katika wilaya za Longido na Monduli.

Mwenyekiti wa kijiji cha Ngoswak, Keryan Lemndoo, amesema mradi wa kaboni umewapa wakazi sababu ya kuhifadhi maeneo ya malisho, kutumia mbinu za kisasa za ufugaji na kupunguza umbali wa kutoka eneo moja hadi jingine kutafuta malisho ya kijani.