Tanzania yashinda kesi ya madai Marekani

Muktasari:
- Mahakama nchini Marekani yatupilia maombi ya familia ya mfanyabiashara Valambhia dhidi ya Serikali ya Tanzania
Serikali ya Tanzania imeshinda kesi ya madai ya dola za Marekani 55 milioni iliyofunguliwa na familia ya aliyekuwa mfanyabiashara Vipula Valambhia ambaye sasa ni marehemu.
Taarifa iliyotolewa jana Ijumaa Aprili 5, 2019m na ofisi ya wakili mkuu wa Serikali imeeleza kesi hiyo ya madai namba 1:18-CV-370(TSC) ilifunguliwa Februari 12, 2018 katika Mahakama ya Columbia nchini Marekani dhidi ya Serikali ya Tanzania pamoja na walalamikiwa wengine ambao ni Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.
Katika shauri hilo walalamikaji wakiongozwa na mjane wa Valambhia, Priscilla Valambhia waliiomba mahakama ya Marekani iweze kutambua na kutoa amri ya kukazia malipo ya fedha kiasi hicho cha fedha zilizoamuliwa na Mahakama Kuu ya Tanzania mwaka 2003.
Walalamikaji hao walidai kiasi hicho cha fedha kilipaswa kulipwa tangu Juni 4, 2001 pamoja na riba ya asilimia saba kila mwaka hivyo wakati wa kufungua shauri hilo deni halisi lilikuwa dola za Marekani 64 milioni.
Madai katika shauri hilo yalitokana na mkataba wa ununuzi wa vifaa vya kijeshi kati ya kampuni ya Transport Equipment Ltd (TEL) ya Valambhia na Serikali ya Tanzania ulioingiwa miaka ya 1980 hata hivyo kampuni hiyo ilidai kuwa haijakamilishiwa malipo yote ya fedha yaliyotokana na mkataba huo.
Serikali ya Tanzania iliwasilisha utetezi wake kupinga shauri hilo Julai 13, 2018 ikipinga madai hayo na kueleza kuwa yalifunguliwa kinyume cha sheria na taratibu za sheria za Marekani inayotambua na kuruhusu kukazia hukumu za kimahakama zinazotokana na uamuzi wa mahakama za nchi nyingine.
Machi 31, 2019 mahakama hiyo ya Colombia ilitoa uamuzi wake na kuona kuwa madai yaliyowasilishwa na familia ya Valambhia hayakuhusisha shughuli za kibiashara zilizofanyika nchini Marekani kama ambavyo sheria ya nchi hiyo inavyotaka.