Lukuvi: Nilijua nitakuwa 'Spika' wa kwanza kukalia kiti hiki
Muktasari:
- Mkutano wa Bunge la 13, kikao cha 1 umeanza leo Jumanne Novemba 11, 2025. William Lukuvi amekalia kiti cha kumpata Spika wa Bunge la Tanzania. Wagombea sita wanachuana kwenye nafasi hiyo kumrithi Dk Tulia Ackson ambaye alijitoa kwenye mbio za kutetea nafasi hiyo.
Dodoma. Mbunge mteule wa Isimani (CCM), Mkoa wa Iringa, William Lukuvi amekanusha uvumi ulioenea mitandaoni kuwa aligombea nafasi ya Spika wa Bunge.
Lukuvi ametoa kauli hiyo leo Jumanne Novemba 11, 2025 wakati akitoa maelezo baada ya kuteuliwa kuongoza uchaguzi wa Spika wa Bunge nafasi aliyoipata kutokana na uzoefu wake ndani ya chombo hicho.
Hata hivyo, Lukuvi amesema alitambua angekalia kiti cha Spika kabla ya kuchaguliwa kwa Spika mpya ambaye atakwenda kukalia kiti hicho.
Lukuvi amepewa heshima hiyo ambapo kanuni huwa zinamruhusu Mbunge aliyekaa bungeni kwa muda mrefu mfululizo.
Mbunge huyo aliingia kwa mara ya kwanza bungeni mwaka 1995 ambapo kulikuwa na uchaguzi wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi.
"Naomba kufuta uvumi ambao ulienea mitandaoni kuwa nimegombea kiti cha Spika, naomba niseme sikugombea na sikutamani kugombea, ila nilijua ningekalia kiti hiki kama 'Spika' wa kwanza kabla ya Spika atakayechaguliwa," amesema Lukuvi.
Ametumia nafasi hiyo kuwashukuru wapiga kura wa jimbo lake kwa jinsi walivyomchagua kwa kura nyingi katika uchaguzi mkuu uliofanyika Oktoba 29, 2025.
Uchaguzi wa Spika unaendelea ambapo wagombea wapo sita akiwemo Mussa Zungu wa Chama cha Mapinduzi (CCM).
Wengine ni Veronica Tyeah (NRA), Aniytha Mgaya (NLD), Chrisant Nyakitita (DP), Ndonge Said Ndonge (AAFP) na Amin Yango wa ADC.
Kwa sasa wagombea hao wanajinadi mmojammoja. Baada ya uchaguzi na kumpata Spika kinachofuata itakuwa ni kiapo kwa wabunge wateule.
Endelea kufuatilia Mwananchi