Russia yadai kuharibu ndege 36 za Ukraine

Picha na mtandao

Muktasari:

  • Gavana wa Jiji la Voronezh, Aleksandr Gusev amesema ulinzi wa anga umeharibu ndege hizo kadhaa za Ukraine japokuwa hakukuwa na majeruhi au uharibifu uliojitokeza.

Moscow. Wizara ya Ulinzi ya Russia imesema vikosi vyake vimeharibu ndege zisizo na rubani 36 za Ukraine katika maeneo ya karibu na mpaka wa nchi hiyo.

Wizara hiyo imesema leo Jumapili, Juni 30, 2023 kwamba: "Mifumo ya ulinzi wa anga iliyokuwa zamu iliharibu UAV 15 katika eneo la Kursk, UAV tisa eneo la Lipetsk, UAV nne kila moja katika mikoa ya Voronezh na Bryansk na UAV mbili kila moja katika maeneo ya Oryol na Belgorod."

Akinukuliwa na Shirika la Habari la AFP, Gavana wa Voronezh, Aleksandr Gusev amesema ulinzi wa anga umeharibu ndege hizo kadhaa japokuwa hakukuwa na majeruhi au uharibifu uliojitokeza.

Tangu kuanza kwa mzozo kati ya nchi hizo baada ya uvamizi wa Februari 2022, pande zote mbili zimekuwa zikitumia ndege zisizo na rubani katika kushambuliana ikiwa ni pamoja na meli kubwa.

Hata hivyo, Ukraine imeongeza mashambulizi yake katika eneo la Russia mwaka huu, ikilenga maeneo yote mawili ya nishati ambayo inasema yanachochea mashambulizi dhidi yao.

Rais wa Russia, Vladimir Putin alianzisha mashambulizi mapya ya ardhini katika eneo la Kaskazini Mashariki la Kharkiv nchini Ukraine mwezi uliopita.

Ameielezea hatua hiyo kuwa ni  operesheni ya kuunda eneo la kuzuia na kuvirudisha vikosi vya Ukraine ili kulinda mpaka wa nchi hiyo kwenye  eneo la Belgorod dhidi ya mashambulizi ya makombora.