Prime
Maeneo ya kijeshi yanayolindwa zaidi duniani-3
Muktasari:
- Licha ya makao makuu ya kijeshi na vituo vya kimkakati kuwa muhimu, wakati huohuo ni chanzo cha taharuki kubwa.
Dar es Salaam. Iwapo Pentagon inawakilisha moyo wa kiutawala wa nguvu za kijeshi za Marekani, basi kuna kundi lingine la miundombinu ya kijeshi kwingineko duniani ambalo limejengwa kwa kusudi tofauti.
Haya si maeneo yaliyoundwa kwa ajili ya shughuli za kila siku za kupanga sera za ulinzi au kusimamia operesheni za kawaida za kijeshi. Badala yake, yameandaliwa kwa ajili ya kukabiliana na nyakati mbaya zaidi ambazo mwanadamu anaweza kukumbana nazo katika historia yake.
Ni vituo vilivyobuniwa kuendelea kufanya kazi hata baada ya kutokea kwa mashambulizi ya nyuklia, mashambulizi makubwa ya kimtandao dhidi ya miundombinu ya taifa au mashambulizi yanayolenga kuangamiza uongozi na mfumo mzima wa amri wa kijeshi wa nchi husika.
Kiwango cha usalama wa maeneo haya hupimwa kwa uwezo wake wa kuhimili mawimbi ya mlipuko wa nyuklia na kwa hesabu za kimkakati zinazofanywa na maadui zake wanapotafakari kama kuyashambulia kunaweza kuleta manufaa yoyote, ikilinganishwa na madhara yatakayofuata.
Historia ya vituo hivi, vilivyotawanyika katika mabara mbalimbali, vilivyozikwa chini ya milima mikubwa au kufichwa ndani ya kina cha bahari, ni historia ya namna ambavyo nguvu za kijeshi zimejengewa makazi ndani ya mandhari ya dunia yenyewe.
Kila kituo ni jibu kwa tishio fulani mahsusi lililobuniwa katika kipindi maalumu cha historia ya mikakati ya kijeshi. Kila kimoja kinaonesha ukweli muhimu kuhusu uhusiano uliopo kati ya mamlaka ya dola, hofu ya kiusalama na hatua za kipekee ambazo mataifa yako tayari kuzichukua ili kulinda uwezo wao wa kutumia na kusimamia nguvu za kijeshi kwa utaratibu uliopangwa.
Cheyenne Mountain, Colorado
Takribani futi 1,100 chini ya mwamba wa Mlima Cheyenne, katika jimbo la Colorado nchini Marekani, kuna moja ya mafanikio makubwa ya kihandisi yaliyofanywa katika kipindi cha vita baridi.
Kituo cha Cheyenne kilijengwa kati ya mwaka 1961 na 1966 kwa gharama iliyokadiriwa kufikia Dola milioni 142 za wakati huo, kiwango ambacho, kwa thamani ya fedha za sasa, kinakaribia Dola bilioni 1.4.
Kilibuniwa kwa lengo la kuendelea kusimama na kufanya kazi hata kama shambulio la nyuklia lingetokea karibu kiasi cha kuangamiza kabisa Jiji la Colorado Springs.
Ujenzi wake ulihitaji uchimbaji wa takribani tani 693,000 za mwamba, kujenga majengo 15 ya chuma ndani ya mlima na kusimikwa juu ya chemchemi maalumu 1,319 zinazoweza kufyonza mawimbi ya mshtuko wa milipuko mikubwa, pamoja na kufunga milango ya kinga inayohimili milipuko yenye uzito wa tani 25 kila mmoja, ambayo inaweza kufunga njia kuu za kuingia ndani ya kituo hicho kwa muda wa sekunde chache tu.
Kwa sasa, kituo hicho hutumika kama makao mbadala ya Norad (Kamandi ya Ulinzi wa Anga na Anga za Juu ya Amerika Kaskazini), pamoja na Kamandi ya Kaskazini ya Marekani, huku makao yao makuu ya kawaida yakiwa katika Kituo cha Jeshi la Anga cha Peterson kilichopo karibu na eneo hilo.
Kituo hicho kina mfumo wake wa kujitegemea wa kuzalisha umeme, vyanzo vya maji na akiba ya mafuta inayoweza kuendeleza shughuli za kila siku kwa takribani siku 30 bila kuhitaji msaada wa vifaa au mahitaji kutoka nje.
Kituo cha Kings Bay, Georgia
Katika pwani ya jimbo la Georgia nchini Marekani, kando mwa Mto St. Marys na Ghuba ya Cumberland, kuna eneo ambalo umuhimu wake wa kimkakati ni mkubwa katika ulimwengu wa kisasa wa kijeshi.
Hapo ndipo kilipo Kituo cha Jeshi la Wanamaji cha Manowari cha Kings Bay, makao makuu ya upande wa Atlantiki ya manowari zinazobeba makombora ya balistiki.
Manowari hizi ndizo zinazobeba takribani asilimia 70 ya vichwa vya nyuklia vya Marekani vilivyowekwa tayari kwa matumizi ya kijeshi.
Mfumo wa ulinzi wa kituo hicho umeundwa kwa kuzingatia uzito na unyeti wa vifaa vinavyohifadhiwa humo. Ndani ya eneo hilo kuna Kituo cha Kimkakati cha Silaha cha Atlantiki, ambacho kina jukumu la kuhifadhi, kuhudumia na kupakia makombora ya Trident pamoja na vichwa vyake vya nyuklia. Kuingia katika kituo hiki kunadhibitiwa kwa viwango vya juu vya usalama.
Kituo cha Yulin
Katika ncha ya kusini ya Kisiwa cha Hainan nchini China, kuna kituo cha kijeshi ambacho kwa muda mrefu kilijengwa kwa usiri na baadaye kikafichuliwa kwa ulimwengu kupitia picha za satelaiti.
Hiki ni Kituo cha Jeshi la Wanamaji cha Yulin, ambacho upanuzi wake mkubwa katika miongo miwili ya kwanza ya karne ya 21 umebadili kwa kiasi kikubwa mizani ya kimkakati katika ukanda wa Pasifiki.
Moja ya sifa zake za kipekee ni mtandao wa vichuguu vikubwa vilivyochongwa moja kwa moja ndani ya milima inayotazama Bahari ya Kusini ya China.
Vichuguu hivyo vina ukubwa unaotosha kuhifadhi manowari za nyuklia zisionekane na mifumo ya ufuatiliaji wa satelaiti za kijeshi.
Kituo hiki kinaipa China uwezo wa kuzifikisha manowari zake za nyuklia moja kwa moja kwenye kina kirefu cha Bahari ya Kusini ya China, ambako zinaweza kufanya doria za kimkakati za kuzuia mashambulizi ya adui. Kwa kutumia makombora mapya yenye uwezo mkubwa zaidi wa kufika mbali, baadhi ya manowari hizo zinaweza hata kushambulia maeneo mbalimbali ya Bahari ya Pasifiki.
Mlima Yamantau, Russia
Katika sehemu ya kusini ya Milima ya Ural nchini Russia, karibu na mji wa Beloretsk katika Jamhuri ya Bashkortostan, kuna Mlima Yamantau, ambao kwa miongo kadhaa umeendelea kuwa chanzo cha maswali, nadharia mbalimbali, juhudi za ukusanyaji wa taarifa za kiintelijensia na hata mahojiano ya kidiplomasia kati ya mataifa makubwa.
Picha za satelaiti za Marekani zilianza kufichua uwapo wa shughuli kubwa za ujenzi kwenye Mlima Yamantau katika miaka ya 1990, chini ya utawala wa Boris Yeltsin.
Tangu wakati huo, swali la nini hasa kilikuwa kinajengwa ndani ya mlima huo, na kwa sababu gani, limeendelea kuwa moja ya mafumbo katika historia ya ujasusi wa kipindi kilichofuata baada ya kumalizika kwa vita baridi.
Kile ambacho kimebainika hadharani ni kwamba shughuli za ujenzi katika eneo la Yamantau zimeendelea kwa muda wa miongo kadhaa.
Mwishoni mwa miaka ya 1990, Bunge la Marekani lilianza kuhoji kuhusu Yamantau, huku maofisa wa Marekani wakitumia nyakati mbalimbali kuwauliza wenzao wa Russia kuhusu madhumuni halisi ya kituo hicho.
Hata hivyo, majibu yaliyotolewa hayakuwa na msimamo mmoja. Wakati mwingine maofisa wa Russia walieleza kuwa ni mradi wa uchimbaji madini, wakati mwingine walidai ni ghala la kuhifadhi chakula, pia wakasema ni eneo la kuhifadhi hazina muhimu za taifa.
Lipi la kujiuliza?
Je, uwepo wa vituo hivi unatueleza nini kuhusu dunia tunayoishi leo?
Kwa kiwango kimoja, jibu ni rahisi. Mataifa yenye uwezo mkubwa wa kijeshi huwekeza rasilimali nyingi katika kulinda miundombinu. Hili ni jambo ambalo limekuwapo tangu nyakati za kale. Kama ilivyokuwa kwa kambi zilizojengewa ngome za majeshi ya Dola ya Roma, ndivyo ilivyo kwa Cheyenne Mountain, Yulin au vituo vingine vya kisasa.
Nguvu za kijeshi zimekuwa zikihitaji vituo salama, njia za ugavi zinazolindwa na makao ya amri yaliyoimarishwa dhidi ya mashambulizi. Tofauti kubwa ni kwamba matoleo ya kisasa ni ghali zaidi, yanatumia teknolojia za hali ya juu na yana athari kubwa kwa usalama wa dunia.
Lakini kuna jibu jingine linalojitokeza pale mtu anapotafakari kwa makini usanifu wa vituo hivi. Kila kimojawapo kiliundwa ili kuendelea kufanya kazi baada ya kila kitu kingine kushindwa.
Katika hali kama hizo, uamuzi utakaofanywa ndani ya vituo hivyo unaweza kuamua kama maafa yatabaki ndani ya mipaka inayoweza kudhibitiwa au kama yataongezeka na kuwa janga lisilo na mfano wowote katika historia ya binadamu.
Hiki ndicho kinachofanya makao makuu ya kijeshi na vituo vya kimkakati kuwa muhimu, lakini wakati huohuo kuwa chanzo cha taharuki kubwa.
Uwapo wake unawatumia wapinzani ujumbe mmoja wa msingi: kwamba uwezo wa kujibu shambulio bado upo, unaweza kuaminika na unaweza kuendelea kuwapo hata baada ya kupigwa.
Tafakuri ya kina
Pentagon ilijengwa ndani ya miezi 19 kwa sababu taifa lilihisi kuwa halikuwa na muda wa kupoteza. Cheyenne Mountain ilijengwa ndani ya miaka kwa sababu silaha zenye nguvu zaidi kuwahi kutengenezwa zilifanya kila jengo lililokuwa juu ya ardhi kuwa mwathirika mtarajiwa.
Manowari za Kings Bay huzama chini ya mawimbi ya bahari kwa sababu mkakati wa kuzuia vita unahitaji kuwapo kwa uwezo wa kulipiza kisasi ambao hakuna adui anayeweza kuuharibu kwa uhakika.
Na mahali fulani ndani ya Mlima Yamantau, shughuli za ujenzi zimeendelea kwa miongo kadhaa kwa sababu Russia, bila kujali mwelekeo wake wa sasa wa kimkakati, inaelewa mantiki ileile iliyowahi kueleweka na kila taifa lililowahi kumiliki silaha za maangamizi makubwa: kwamba uwezo wa kustahimili shambulio na bado kuweza kujibu ndiyo bima pekee yenye thamani ya kweli.
Ni nini kinachofanya vituo hivi kuwa muhimu kiasi kwamba mataifa yote hutumia rasilimali kubwa kuvilinda?
Jibu si la kimkakati pekee. Vituo hivi hulinda uwezo wa kufanya uamuzi; yaani, mamlaka ya kibinadamu ya kuamua hatua ya kuchukua katika nyakati za hatari kubwa zaidi. Kila kitu kingine; walinzi, milango ya kuzuia milipuko, mitandao inayoendeshwa kwa siri kubwa na hata milima mikubwa inayovifunika; kipo kwa lengo moja kuu: kuhakikisha kwamba mamlaka hiyo inaendelea kuwapo.
Katika dunia ambayo uwezekano wa tukio baya zaidi haujawahi kutoweka kabisa, hilo ndilo swali ambalo linaendelea kubaki daima bila kupoteza umuhimu wake.