Theluthi moja ya migebuka ya Tanzania inauzwa nje ya nchi

Muktasari:

  • Tanzania ndiyo mzalishaji mkubwa wa dagaa, lumbu na mgebuka, imeeleza ripoti ya mnyororo wa thamani wa dagaa, lumbu na mgebuka katika Ziwa Tanganyika nchini.

Dar es Salaam. Pamoja na Tanzania kuwa mzalishaji mkubwa wa dagaa, lumbu na mgebuka duniani, ni theluthi moja pekee ndiyo inayouzwa nje ya nchi.

 Kwa mujibu wa ripoti ya mnyororo wa thamani wa dagaa, lumbu na mgebuka katika Ziwa Tanganyika nchini, Tanzania inazalisha tani 48,000 za dagaa na 28,800 za mgebuka, hivyo inachangia asilimia 85 ya uzalishaji duniani kwa mwaka.

Ripoti hiyo ya Desemba mwaka jana, iliyozinduliwa leo, Machi 21, 2023 inaeleza samaki hao wanauzwa katika mataifa ya Burundi, Jamhuri ya Demokrasi ya Congo na Zambia.

"Usafirishaji nje ya nchi wa dagaa, lumbu na mgebuka ulikuwa na thamani ya Dola 870,000 za Marekani kwa mwaka 2021," imeeleza sehemu ya ripoti hiyo iliyofanywa na Shirika la Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) kwa kushirikiana na Shirika la Chakula Duniani (FAO) na Umoja wa Ulaya (EU),.

Hata hivyo, inabainisha uwepo wa upotevu wa mazao, kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi na njia duni za uvuvi

Kulingana na ripoti hiyo iliyofanywa chini ya mradi wa FISH4ACP wa Umoja wa Afrika na Pasifiki, theluthi mbili ya samaki hao wanauzwa ndani.

Ripoti hiyo iliyofanywa na Shirika la Utafiti wa Uvuvi (TAFIRI) kwa kushirikiana na Shirika la Chakula Duniani (FAO) na Umoja wa Ulaya (EU), imesema wanaouzwa ndani ni katika masoko ya mtaani.


"Samaki hao wanauzwa wakiwa wabichi katika masoko ya mitaani na waliobanikwa, kukaushwa kwa jua au waliogandishwa barafu wanauzwa kwa matumizi ya ndani," imeeleza sehemu ya ripoti hiyo.

Akizungumza baada ya uzinduzi wa ripoti hiyo, Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Profesa Rizik Shemdoe amesema kinachofanywa na Serikali ni kuangalia maoungufu yaliyopo kwenye mnyororo wa thamani wa dagaa na mgebuka.

"Tunahangaika ubora na maeneo yenye changamoto kwenye mnyororo wa thamani wa dagaa na mgebuka kwa ajili ya kuangalia namna ya kupata suluhu itakayowezesha mchango mkubwa katika uchumi wa nchi," amesema.

Amesema pamoja na uzinduzi wa ripoti hiyo, pia inafanyika warsha ya kuandaa mpango wa kusaidia utekelezaji wa mapungufu yaliyobainika kwenye mnyororo wa thamani.