Historia ya kibabe, Tanzanite Queens ikifuzu Kombe la Dunia
Baadhi ya wachezaji wa kikosi cha Tanzanite Queens. Picha na Mtandao
Muktasari:
- Kocha Mkuu wa Tanzanite Queens, Bakari Shime anaandika rekodi ya kuwa kocha pekee wa soka Tanzania kuwahi kuzipeleka timu mbili za taifa katika fainali za Kombe la Dunia.
Timu ya Taifa ya Wanawake chini ya umri wa miaka 20 ‘Tanzanite Queens’ imefanikiwa kutinga Fainali za Kombe la Dunia baada ya leo, Jumapili, Mei 10, 2026 kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Cameroon.
Ushindi huo umeifanya Tanzanite Queens ifuzu kwa kubebwa na faida ya bao l ugenini baada ya michezo miwili kati ya timu hizo kumalizika kwa sare ya mabao 3-3.
Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Yaounde, Cameroon, wenyeji waliibuka na ushindi wa mabao 3-1.
Walioitoa kimasomaso Tanzanite Queens katika mchezo wa leo ni Mary Aron na Hasnath Ubamba ambao kila mmoja alifunga bao.
Tanzanite Queens sasa imefikia rekodi iliyowahi kuwekwa na timu ya Taifa ya wanawake ya vijana chini ya umri wa miaka 17 'Serengeti Girls' na ile ya timu ya taifa ya Wanawake ya Futsal ya kuwa timu pekee za taifa za Tanzania zilizowahi kufuzu Fainali za Kombe la Dunia chini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani (FIFA).
Serengeti Girls ilishiriki Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2022 na kuishia katika hatua ya robo fainali wakati katika Kombe la Dunia la Wanawake la Futsal, Tanzania iliishia katika hatua ya makundi.
Kocha Mkuu wa Tanzanite Queens, Bakari Shime anaandika rekodi ya kuwa kocha pekee wa soka Tanzania kuwahi kuzipeleka timu mbili za taifa katika fainali za Kombe la Dunia.
Shime ndiye pia aliiongoza Serengeti Girls kufuzu Fainali za Kombe la Dunia mwaka 2022 zilizofanyika India.
Lakini pia Uwanja wa New Amaan Complex umeendeleza historia nzuri ya kuzibeba timu za Tanzania katika kufuzu kwenda hatua muhimu za mashindano mbalimbali.
Ni uwanja huohuo ambao Serengeti Girls ilicheza mechi iliyoiwezesha kwenda Kombe la Dunia lakini pia Simba ilipata ushindi dhidi ya Stellenbosch uliochangia kwa kiasi kikubwa itinge fainali ya Kombe la Shirikisho Afrika msimu uliopita.
Safari ya Tanzanite Queens kufuzu Kombe la Dunia mwaka huu ilianzia raundi ya pili baada ya kuitupa nje Angola kwa ushindi wa jumla wa mabao 7-0, ikishinda mabao 4-0 katika mechi ya kwanza na marudiano ikashinda mabao 3-0.
Katika raundi ya tatu, iliitoa Kenya kwa mikwaju ya penalti 3-1 baada ya mechi mbili baina ya timu hizo kumalizika kwa sare ya bao 1-1 na raundi ya mwisho ndio ikaitoa Cameroon.
Fainali za Kombe la Dunia kwa Wanawake chini ya umri wa miaka 20, zitashirikisha idadi ya timu 24 zitakazogawanywa katika makundi sita yenye timu nne kila moja.