Crystal Palace yatwaa Europa Conference League ikiendeleza heshima England
Muktasari:
- Ni taji la tatu kwa Glasner kuipatia Crystal Palace ndani ya muda usiozidi miezi 12 kwani pia aliwapatia Kombe la FA msimu uliopita na Ngao ya Jamii kabla ya kuanza kwa msimu huu.
Crystal Palace imetwaa taji la UEFA Conference League baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Rayo Vallecano katika mechi iliyochezwa Jumatano, Mei 27, 2026 katika Uwanja Red Bull Arena, Leipzig, Ujerumani.
Bao pekee lililoipa taji Crystal Palace limefungwa na Jean-Phillipe Mateta katika dakika ya 51.
Kutwaa taji hilo kwa Crystal Palace ni njia nzuri ya kumuaga meneja wake Oliver Glasner ambaye baada ya mchezo huo ataachana na timu hiyo.
Ni taji la tatu kwa Glasner kuipatia Crystal Palace ndani ya muda usiozidi miezi 12 kwani pia aliwapatia Kombe la FA msimu uliopita na Ngao ya Jamii kabla ya kuanza kwa msimu huu.
Lakini pia ni taji la kwanza la mashindano ya Ulaya kwa Crystal Palace ambayo sasa imejihakikishia kucheza mashindano ya Europa League msimu ujao.
Ni timu ya pili ya England kutwaa taji la mashindano ya Ulaya msimu huu baada ya Aston Villa kufanya hivyo katika Europa League.
England inaweza kuandika historia ya klabu zake tatu kutwaa mataji yote matatu ya Ulaya msimu huu iwapo Arsenal itaibuka na ushindi dhidi ya PSG katika fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya keshokutwa Jumamosi.