KONA YA FYATU MFYATUZI: Yaani mkimbinafsisha Bi Mkubwa namfyutua mtu

Mtukufu Dk Rahis, msikivu, mwenye maono, ndoto, uthubutu, ukimya, nk, naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu, rahis, du! A’udhu billahi min ash-shaytaan-ir-rajeem.

Nimemsahau Mtume! Naona yule anashangaa. Kwani nazusha? Wangapi, sijui chawa, sijui kunguni, wakianza kuchonga wanafanya hivyo kwa maangamizi yao na mafyatu wao?

Nasikia kila mara rahis akisifiwa kuwa na ‘maono’ tena yasiyooneka. Kupitia maono, naona mabos wamegawa, sorry, binafsisha bahari, bandari, barabara, mbuga za waanimo n.k kama ni kweli. Hii inantisha kwelikweli.

Naomba leo nifyatue kitu. Hivi huyu Bi Mkubwa ni Mungu, muungu, malaika, au ntume? Hakosei?

Je, hizi sifa za kweli au kupakana mafuta kwa mgongo wa chupa au uchawa na ukunguni wa kutumia matumbo kufikiri badala ya vichwa ili kujaza matumbo?

Nasikia viongozi mnatenda ‘maajabu’. Je, ni maajabu kweli katenda au ni ajabu kusema katenda? Mnamwaga njuluku. Mafyatu wanazipata? Mnamwaga kiasi gani na kwa yupi? Nasikia watu wanasema tu.

Mnamwaga pikipiki. Tunahoji ni za nini na hiyo njuluku mmeitoa wapi au mnaipataje na anategemea kupata nini na kwa nini sasa tunapoelekea kwenye uchaguzi?

Mnanunua nini? Ajabu, wakati mkitoa pikipiki kwa kila nkoa bwerere, akina maza wenzake wajawazito wanajifungulia nje ya zahanati! Mwe! Kwani hamjui adha ya ujauzito na machungu ya kujifungua? Hayo tuyaache.

Je, viongozi ni matajiri kiasi gani na nini chanzo cha ukwasi, ‘huruma na upendo’ hivi ni vya nini, na mnategemea kupata nini?

Mafyatu tukienda hospitali tunaandikiwa dawa tukanunue! Maji ya mgawo!

Je, hizi njuluku za pikipiki zingesaidia wajawazito, mafyatu, hata upatikanaji wa maji kiasi gani? Je, hii njuluku ingeondosha michango ya hovyo na tozos kiasi gani?

Je, mikoa yetu inahitaji pikipiki wakati pesa inayopata tokana na bajeti ni kiduchu? Kuendesha mangwalangwala ya mwendo kinyonga, sorry, kasi?

Tunapaswa kuwa wakweli. Pia, hizi pikipiki ni za nini kama hakuna namna ya kuhongana, sorry, kuchanganyana, kuelekea kwenye uchakachuaji mwakani?

Kwa nini sasa na si jana wala juzi? Je, nyie mabilionea wa sirini mnalipwa nshahara kiasi gani? Tukiuliza haya, mengine, na mengineyo tunakosea?

Turejee kwenye uwekezaji ambao wapingaji wanauita uchukuaji kama siyo uchakachuaji na uhujumu uchumi uliohalalishiwa na kufanywa na wanene tena kwa mlango wa nyuma.

Bandari, tumewekeza. Juzi tuliona gawio la madafu 153.9 bilioni, sawa na dolari za Kijoji Kichaka milioni 80! Kiduchu hichi kwa mwaka! Je waliingiza kiasi gani tujue kama kweli ni gawio au zenguo?

Tunapaswa tujiulize na kuwauliza wamepata nini na wanatupa nini na nini tulipaswa kupata kisheria na kimakadirio.

Tusifanye magawio kuwa hisani bila kujiridhisha kuwa tunachopata ndiyo stahili yetu badala ya kujiruhusu kupigwa na kufyatuliwa kijiiinga tu.

Fine. Je, kwa namna bandari inavyotema njuluku, kweli tulichopewa ni stahiki au chenga la mato?

Mwaka 2016, bandari iliripoti mapato ya Sh13.37 trilioni (Mwananchi, Julai 6, 2016). Je, kwa gawio hili walipata kiasi gani? Je, walifikia, kutofikia au kuvuka malengo?

Je, hiki ndicho tulichoahidiwa na kutegemea baada ya kugawiwa, sorry, kuuzwa, sorry, kubinafsishwa bandari kwa watasha wa Do Buy?

Barabara tunawekeza baada ya kuunguza njuluku ndefu za mafyatu kuzitengeneza ili kuwanufaisha wachache?

Nafyatua maswali yote haya na mengine kuepuka kuuziwa goat kwenye gunia tunajiona.

Bahari, tumebinafsisha. Natamani na visiwa vibinafsishwe uone Wazenj watakavyocharuka na kudai uhuru. Natamani hata makaburi yabinafsishwe.

Bado milima na mito. Tukimaliza yote haya, tunabinafisha na machawa. Sijui nani atakuwa tayari kuwanunua wamkondeshe kama mafyatu.

Tukimaliza vyote kweli kesho hamtabinafsisha hata hewa?

Je, Wakubwa zetu watanusurika? Wallahi, ikifikia kubinafisishana na mkamgusa Bi Mkubwa wangu–tate nane tate nane–nakufa na fyatu. Hata hivo, kabla ya kumfyatua fyatu, Nimesemeje? We koma!

Najua Ngolongolo akina Yero weshabinafsishwa na kuhongwa, sorry, kujengewa vibanda kule Msomea.

Ukisikia maono ya viongozi na wamanga ndiyo haya. Si juzi niliowaona wakiwa wameishakubuhu kukata vikalio utadhani walizaliwa Tangamano. Huo nao uwekezaji au siyo.

Soon, nitawaona wamanga wamepiga migolole ya kiyero wakipambana na lion. Nao ni uwekezaji au siyo.

Nimalizie. Hata kama mnatuaminisha hata kutufyatua kuwa uwekezaji ni muhimu kama kweli ni uwekezaji kama siyo uchukuaji, basi wekezeni kwa busara, tushirikishe, msituhamishe na kutuchuuza kama ilivyo sasa.

Pia, wajibikeni na kueleza mnavyotumia njuluku zetu na zenu kama mnazo kama kwenye skandali ya pikipiki.

Hivi niko wapi? Kama naota!