Serikali yamwaga ajira mpya kwa walimu, afya 21,200

Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, Angela Kairuki akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatano Aprili 12,2023 jijini Dodoma. Picha na Tamisemi

Muktasari:

  • Serikali imetangaza ajira 21,200 kwa kada za walimu na afya ambazo maombi yake yanaanzia leo hadi Aprili 25,2023.

Dodoma. Serikali imetangaza ajira 21,200 kwa kada za walimu na afya ambazo maombi yake yanaanzia leo hadi April 25,2023.

 Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, Angela Kairuki ametangaza nafasi hizo leo Jumatano Aprili 12,2023 alipozungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma.

Waziri Kairuki ametaja mgawanyo wa nafasi hizo ni 13,130  ambazo zitachukuliwa na walimu wa shule za msingi na Sekondari huku afya ikitengewa nafasi 8,070 kwa watumishi wa ngazi ya zahanati, vituo vya afya na Hopsitali.

Waombaji ni wahitimu wa nafasi hizo kuanzia mwaka 2015 hadi 2022 ambao watakuwa na sifa stahiki na wasiozidi umri wa miaka 45 lakini wanaofanya kazi za kujitolewa wameitwa kuomba nafasi hizo bila kusema kama watapewa kipaumbele.

“Rais ametoa kibali cha kuajiri watumishi hao nasi tunaanza mchakato huo mara moja kuanzia leo, wanaoajiriwa ni kuanzia ngazi ya cheti hadi Shahada kulingana na kada anayoiomba mhusika,” amesema Kairuki.

Hata hivyo ameonya waombaji watakaodanganya sifa zao katika maombi ikiwemo wenye ulemavu ambao wametengewa nafasi na watakaogushi umri kwani Serikali inachukua watumishi wasiozidi miaka 45.

Amesema waombaji wote wataomba kupitia mtandao wa Tamisemi na waliokuwa wameomba siku nyingi wametakiwa kuhuisha taarifa huku akitoa katazo la waombaji ambao watatuma maombi yao kwa njia ya barua au posta kwamba hayatapokelewa.