Sh2.2 bilioni kupunguza maumivu ukosefu wa ajira, Dar

Katibu Tawala Msaidizi uzalishaji na uchumi Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam,Dk Elizabeth Mshote  akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa uwezeshaji vijana iliyoandaliwa na Benku ya Standard Chartered jijini Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Wakati vilio vya kukosekana kwa ajira vikiendelea miongoni mwa vijana, benki ya Standard Chartered imepanga kutumia zaidi ya Sh2.2 bilioni katika utekelezaji wa programu ya uwezeshaji vijana kiuchumi ili kupunguza kukabili hiyo.

Fedha hizo zitatumika katika kusaidia vijana kupata ujuzi ikiwa ni maandalizi ya kupata ajira na kusaidia usimamizi wa biashara ndogo kupitia mradi wa Future Makers.

Akizungunza katika hafla ya uzinduzi wa peogramu hiyo, Katibu Tawala Msaidizi idara ya uzalishaji na uchumi Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Dar es Salaam, Dk Elizabeth Mshote alisema kupitia mradi huo vijana 270 wenye ulemavu watasaidiwa kupata ujuzi kama maandalizi ya kupata ajira.

Kwa upande wa wajasiriamali mradi huo unatarajia kunufaisha biashara 90 ikiwemo suala la ushauri, utaalamu wa kibiashara katika kukuza biashara zao na kuwezesha biashara ndogondogo kutengeneza fursa fursa za ajira 144.

“Hii ni fursa kubwa sana, Serikali inathamini na kuipongeze benki ya Standard Chartered kwa kuwezesha Sh2.2 bilioni na tunaamini mradi huu utasaidia kupunguza changamoto za ajira na ujasiriamali katika kundi la vijana,” alisema Dk Elizabeth.

Mkurugenzi wa Chama cha Waajiri Tanzania (ATE), Dk Susan Ndomba alisema “Mpango unaojumuisha watu wenye ulemavu, usawa wa kijinsia na vijana na makundi maalumu ni muhimu sana katika maendeleo ya nchi yetu”