Baada ya Maradona amekuja Messi, nani baada yake?
Muktasari:
- Siku hiyo, Messi alikosa penalti na kuifanya Argentina ipoteze fainali yake ya nne ndani ya miaka tisa. Hali hiyo ilimfanya ashindwe kuvumilia maumivu hayo.
MWAKA 2016, Lionel Messi alitangaza kustaafu kuchezea timu ya taifa ya Argentina, hiyo ni baada ya kufungwa na Chile katika fainali ya Copa America.
Siku hiyo, Messi alikosa penalti na kuifanya Argentina ipoteze fainali yake ya nne ndani ya miaka tisa. Hali hiyo ilimfanya ashindwe kuvumilia maumivu hayo.
“Kwa upande wangu, safari yangu na timu ya taifa imekwisha. Nimefanya kila nilichoweza. Inauma kutokuwa bingwa,” alisema Messi wakati huo.
Ni vigumu kufikiria kwamba miaka 10 baadaye, yaani siku mbili kabla ya kutimiza miaka 39, si tu kwamba Messi bado angekuwa akiichezea Argentina ambayo ni bingwa mtetezi wa Kombe la Dunia, bali pia angekuwa mfungaji bora wa muda wote katika historia ya michuano hiyo.
Uamuzi wake wa kubadili mawazo na kurejea katika timu ya taifa umezaa kipindi cha mafanikio makubwa kwake na Argentina kwa ujumla.
Tangu hapo, Argentina imeshinda mataji mawili yaliyopita ya Copa America na mwaka 2022, Messi aliiongoza nchi hiyo kutwaa Kombe la Dunia, akifunga mabao saba, yakiwemo mawili katika fainali dhidi ya Ufaransa, huku Argentina ikitwaa taji hilo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1986 ambapo pia likiwa la tatu.
Jumatatu ya Juni 22, 2026, miaka 40 kamili tangu Diego Maradona afunge mabao mawili katika ushindi wa 2-1 dhidi ya England kwenye robo fainali ya Kombe la Dunia 1986 pale Estadio Azteca, Mexico City, Messi ameendelea kuandika historia mpya kwa kufunga mabao yote mawili katika ushindi wa 2-0 dhidi ya Austria, ikiwa mechi ya Kundi J iliyochezwa Uwanja wa Dallas, Marekani.
“Nafurahia kucheza na kufurahia muda wangu uwanjani. Tunafurahia pia kuona watu wakifurahia namna hii na kuwapa furaha ya aina hii,” anasema Messi.
Kukosa penalti katika dakika ya nane ya mchezo huo haukuwa mwanzo mzuri kwake, lakini dakika 30 baadaye alisahihisha kosa hilo kwa kufunga bao la shuti la chini lililokuwa la 17 kwake katika Kombe la Dunia, na kumvuka Miroslav Klose wa Ujerumani kama mfungaji bora wa muda wote katika historia ya mashindano hayo.
Bao la 18 halikuchukua muda mrefu kufika, kwani Messi alifunga tena katika dakika za nyongeza kipindi cha pili, akipenyeza mpira kati ya mabeki wawili wa Austria.
“Muda hautoshi kujenga sanamu za Lionel Messi au kuandika uchambuzi wa kina kuhusu yeye kwenye magazeti. Hatuwezi kwenda sambamba naye,” anasema mwandishi wa habari za soka wa Hispania, Guillem Balague, kwenye BBC Radio 5 Live.
Kwa sasa Messi ana mabao 18 katika mechi 28 za Kombe la Dunia. Itakuwa vigumu kubashiri kwamba hataongeza idadi hiyo, hasa kwa kuwa Argentina bado inakabiliwa na Jordan huku ikiwa tayari imefuzu hatua ya mtoano ya timu 32 bora.
Messi anashiriki Kombe la Dunia kwa mara ya sita kuanzia 2006 na amefunga mabao 13 katika mashindano hayo tangu alipoamua kurejea kutoka kustaafu kuchezea timu ya taifa.
Cha kushangaza zaidi, mabao 12 kati ya 18 aliyofunga kwenye michuano hiyo yamepatikana baada ya kutimiza miaka 35. Mabao 14 kati ya hayo 18 ameyafunga kwa mguu wa kushoto anaoutumia zaidi, huku manne akiyafunga nje ya eneo la penalti.
“Anafurahia mchezo na hicho ndicho kitu muhimu zaidi. Nimewahi kumuona kwenye Kombe la Dunia ambapo hakuweza kumaliza dakika 90. Lakini sasa hata mwisho wa mchezo alikuwa akikimbia kama wengine. Anaielewa vyema sana miili yake.
“Messi hahitaji kukimbia sana. Hata kasi kubwa ya ghafla hahitaji ili kuwazidi mabeki, anatumia akili yake. Nafikiri tutamuona tena hata baada ya miaka minne,” anabainisha Balague.
Takwimu zake zinaendelea kuvutia zaidi. Amefunga mabao yote matano ya Argentina katika Fainali za Kombe la Dunia mwaka huu na anaongoza orodha ya wafungaji kwa tofauti ya bao moja.
Dhidi ya Austria, amekuwa mchezaji wa tatu kufunga katika mechi sita mfululizo za Kombe la Dunia baada ya Just Fontaine mwaka 1958 na Jairzinho mwaka 1970.
Mabao yake mawili dhidi ya Austria yalimaanisha alitumia vyema nafasi zake zote mbili za kufunga, huku pia akiwa mchezaji aliyeunda nafasi nyingi zaidi katika historia ya mashindano hayo (76).
Katika mechi sita zilizopita za Kombe la Dunia alizocheza, Messi amehusika moja kwa moja katika mabao 12, akifunga 10 na kutoa pasi mbili za mabao.
“Je, tunamshuhudia mchezaji bora zaidi kuwahi kutokea? Inawezekana na ni mjadala unaostahili kufanyika,” alihoji beki wa zamani wa Wales, Ashley Williams.
“Huenda tumeshuhudia mchezaji bora zaidi katika historia ya soka.”
Kiungo wa zamani wa England, Danny Murphy, alikubaliana na kauli hiyo akisema: “Lionel Messi anaendelea kujikuta katika maeneo sahihi kutokana na uhuru aliopewa uwanjani.
“Uelewa wake wa mchezo ni wa kiwango cha juu sana. Anajua kutafuta nafasi na muda wake wa kufanya uamuzi ni bora. Kwangu ndiye mchezaji bora zaidi niliyewahi kumuona.”
Mshambuliaji wa zamani wa Ufaransa na bingwa wa dunia mwaka 2018, Olivier Giroud, anasema: “Hateseki kimwili. Anaisimamia vyema afya na mtindo wake wa maisha, kwa sababu bila kufanya hivyo huwezi kucheza kwa muda mrefu kiasi hiki.
“Ni wa ajabu. Amebarikiwa uwezo wa kuendelea kucheza mechi baada ya mechi.”
Lakini je, Argentina inamtegemea Messi kupita kiasi?
Mshambuliaji wa zamani wa England, Chris Sutton, anasema: “Uchawi wa Lionel Messi umeonekana tena kwa Argentina. Siyo mabao yake tu, bali mchango wake kwa timu kwa ujumla.
“Namna anavyounganisha mchezo yeye ndiye mtu mdogo kwa nyakati kubwa.
“Labda jambo linaloweza kumtia wasiwasi kocha Lionel Scaloni ni kwamba angependa kuona wachezaji wengine wakichangia mabao. Hawawezi kumtegemea Messi pekee au wanaweza?”Tukio la penalti dhidi ya Austria, lilitokana na Lautaro Martinez kuangushwa eneo la hatari, lakini Messi alipiga mpira nje.
“Kulikuwa na wakati nilikasirika sana kwa sababu nilikosa penalti hiyo na nilijilaumu sana,” anasema Messi.
“Kwa bahati nzuri tuliweza kubadilisha hali hiyo, tukapata bao la kuongoza na kushinda mchezo.”
Hatua hiyo imemfanya Messi kuwa mchezaji wa kwanza kukosa penalti katika Kombe la Dunia 2026 na sasa ndiye mwenye penalti nyingi zaidi zilizopigwa (7) na kukosa nyingi zaidi (3) katika historia ya michuano hiyo kwa ujumla ndani ya muda wa kawaida.
Pia amekosa kufunga penalti sita kati ya 31 alizopiga akiwa na Argentina.
Kwa kufunga mabao mawili dhidi ya Austria baada ya kukosa penalti, huu ulikuwa mchezo wa kwanza wa ushindani ambapo Messi alifunga kwa Argentina baada ya pia kukosa penalti katika mechi hiyo.
“Messi ni binadamu kama wengine, anaruhusiwa kufanya makosa mara chache,” anasema Murphy na kuongeza kwa kutania.
“Labda aliikosa makusudi penalti hiyo. Pengine rekodi hiyo ilipaswa kuvunjwa kwa bao zuri zaidi.”
Mchambuzi wa soka la Amerika Kusini, Tim Vickery, anaongeza kwamba: “Miungu ya soka haikutaka avunje rekodi kwa penalti. Ilitaka avunje rekodi kwa bao la wazi kutoka kwenye mchezo.
“Argentina imeijenga timu yake kumzunguka yeye, na sitaki hili lifike mwisho.”
Licha ya kuwa na rekodi nyingi tayari, bado kuna nyingine za kuvunja.
Rekodi inayofuata inaweza kuwa ya pasi za mabao nyingi zaidi katika historia ya Kombe la Dunia, kwani kwa sasa Messi yuko sawa na Maradona akiwa na pasi nane za mabao.
Mchezo dhidi ya Jordan katika mechi ya mwisho ya hatua ya makundi utampa Messi nafasi nyingine ya kuendelea kuandika historia mpya ya soka? Tusuburi tuone Juni 28, 2026.