Wasimulia raha ya ongezeko shule za kata

Muktasari:

  • Halmashauri ya Mji wa Geita yenye wanafunzi 25,155 ina shule za Sekondari 26 ikiwa ni ongezeko la shule mpya 16 kutoka 10 zilizokuwepo mwaka 2019.

Geita. Ujenzi wa shule mpya za sekondari katika Halmashauri ya Mji wa Geita, umesaidia kupunguza mdondoko wa wanafunzi kutoka 759 mwaka 2019 hadi 338 mwaka 2023 na utoro rejareja kutoka 916 hadi  433 katika kipindi kama hicho.

Pia, umesaidia kupunguza mimba kwa wanafunzi kutoka 17 mwaka 2019 hadi nne mwaka 2023.

Halmashauri ya Mji wa Geita yenye wanafunzi 25,155, ina shule za sekondari 26 ikiwa ni ongezeko la shule mpya 16 kutoka shule 10 zilizokuwepo mwaka 2019.

Akizungumza na Mwananchi Digital leo Jumanne Machi 12, 2024, Ofisa Elimu Sekondari, Rashid Mhaya amesema ujenzi wa shule mpya si tu umepunguza utoro shuleni bali pia umepunguza mimba na kuwaondolea wanafunzi adha ya kutembea umbali mrefu.

Mhaya amesema shule mpya zilizojengwa kwa sasa zina wanafunzi 11,431 ambao ni sawa na nusu ya wanafunzi wote na kuwa awali wanafunzi hao walilazimika kutembea zaidi ya kilomita 16-40 kwa siku kutafuta elimu.

 “Hizi shule zimekuwa na manufaa makubwa, mfano 2019 ziliripotiwa mimba 17 lakini 2023 zimeripotiwa nne tu, utoro ulikuwa asilimia 6.3 na sasa ni asilimia 3 na mdondoko ulikuwa asilimia 4.7 na sasa ni asilimia 3. Kwa sasa wananfunzi wanaoanza na kumaliza ni kiwango kikubwa kuliko ilivyokuwa 2019,”amesema Muhaya.

Akitolea mfano wa Shule ya Shantamain, Muhaya amesema ililazimika kuchukua wanafunzi kutoka kata mbili za Mgusu na Mtakuja ambao walikuwa wakitembea zaidi ya kilometa 30 kwa siku.

Anasema baada ya shule mpya kujengwa katika kata, zimewapunguzia adha ya kutembea umbali mrefu wanafunzi na zimesaidia kupunguza msongamano madarasani na sasa faida wanaiona.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wanafunzi waliopangiwa shule ya Shantamine na kuhamishiwa shule mpya ya Nyantorotoro, wamesema walikua wakilazimika kuamka alfaji kwenda shule umbali wa zaidi ya kilometa 10.

naye Suzy Majaliwa anayesoma Shule ya Shantamine ambayo iko katika Kata ya Nyankumbu, amesema alikuwa hafanyi vizuri darasani kutokana na kuchoka, lakini hivi sasa amepata unafuu mkubwa.

“Sichoki tena kama zamani na akili yangu imetulia, siwazi tena kutembea umbali mrefu, shule imejengwa jirani na nyumbani,” anasema Suzy.

Anasema umbali ulikuwa ukiwalazimisha  kuamka saa 11 alfajiri na kurudi saa 12 jioni, na kuwa vigumu kwao kusoma, pia ilichangia wanafunzi wa kike kushawishiwa na kuacha shule.

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Shantamine, Kapira Swila anasema walimu walikuwa wanakutana na changamoto ya wanafunzi kuchelewa kufika shule, utoro wa rejareja huku kipindi cha mvua wengi wakishindwa kuhudhuria masomo.

Amesema awali, asilimia 40 ya wanafunzi wa kike waliokuwa wakitoka mbali na shule waliacha masomo.

Amesema  ujenzi wa shule na uwepo wa mabweni umechochea ongezeko la ufalu ambapo takwimu za mwaka 2023, wanafunzi wengi wa kike walifaulu zaidi kwa kupata daraja la kwanza hadi la tatu, tofauti na miaka ya nyuma walipokuwa wanapata daraja la nne na sifuri.

Takwimu zinaonyesha wastani wa ufaulu kwa Halmashauri ya Mji wa Geita umeongezeka kutoka  asilimia 85.69 mwaka 2019 hadi kufikia 93.15 mwaka 2023.