Wahamiaji haramu wengine 16 wakamatwa Mufindi, gari yenye namba za Serikali yatumika
Muktasari:
- Dereva atelekeza gari baada ya kuona askari anawafuatilia, awashusha wahamiaji hao msituni.
Iringa. Jeshi la Polisi mkoani Iringa limewakamata wahamiaji haramu 16, raia wa Ethiopia kwa kosa la kuingia nchini bila kibali.
Akizungumza na waandishi wa habari Mjini Mafinga leo Aprili 8,2024 Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP), Allan Bukumbi amesema Jeshi hilo kwa kushirikiana na Jeshi la Uhamiaji mkoani humo, wamefanikiwa kuwakamata wahamiaji hao katika eneo la msitu wa Luganga, kata ya Sao Hill Tarafa ya Ifwagi wilayani Mufindi.
Amesema wahamiaji hao waliwakamata wakiwa wametelekezwa katika shamba la mahindi baada ya kushushwa kwenye gari ambalo awali lilikuwa likisomeka namba za usajili STL 3999 Landcruiser V8 yenye rangi nyeupe.
“Baada ya amelitelekeza gari hilo baada ya kuna anafuatiliwa na askari, akaona hataweza kupitia barabara kuu, hivyo alipita njia nyingine na kufika sehemu ambapo alikutana na tikiti ( swap), alisindwa kuendelea na safari hiyo, ndipo alifikia hatua ya kuwashusha wahamiaji hao na kutokomea kusikijulikana," amesema RPC Bukumbi
Amesema uchunguzi wa awali umebaini gari hiyo imesajiliwa kwa namba T803 CVW inayomilikiwa na Saidi Hassan, mkazi wa Tabata, Dar es Salaam huku akieleza jitihada zinaendelea kumtafuta dereva huyo na mmiliki wa gari hilo.
Kwa upande wake, Kamishna Msaidizi wa Uhamiaji (ACI), Peter Kimario na Ofisa Uhamiaji Mkoa wa Iringa, amesema biashara hiyo haramu ya binadamu ni mbaya, kwani inahatarisha usalama wa Taifa.
"Kupitia vyombo vya habari, nitoe wito kwa wananachi watusaidie katika kampeni yetu ambayo imeanzishwa nchini mzima inayoitwa ‘Mjue jirani yako’ kwa sababu hawa tumewakamtwa kwenye magari ya aina hiyo.
“Hivyo tunaamini wanaweza kutumia mbinu za kuvaa vizuri kama wa Tanzania na kusafiri katika vyombo vya usafiri vya kawaida bila kuwajua," amesema ACI Kimario
Kimario amefafanua kuwa kampeni hiyo imeanzishwa ili kujua vitu vinavyoendelea katika maisha ya wananchi kwa sababu usalama wa nchi kila mtu anahusika.
Hata hivyo, amesema jeshi hilo la uhamiaji litaendelea kushirikiana na vyombo vingine, ili kuhakikisha wahamiaji hao wanafikishwa kwenye vyombo husika na kuchukuliwa hatua.