IMELIPIWA-Ubungo: Halmashauri kinara katika uwezeshaji wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Patrobas Katambi (kushoto) akizungumza na Mkurugenzi wa Manispaa ya Ubungo, Beatrice Dominic alipotembelea baadhi ya vikundi vya vijana vya Manispaa ya Ubungo ambavyo vimenufaika na mikopo ya asilimia 10 wakati wa maadhimisho ya siku ya vijana duniani, 2022.


Muktasari:

Walikuwa ni miongoni mwa vijana waliokuwa na hamasa kubwa ya kujiajiri ili kujipatia kipato cha kue­ndesha familia zao pamoja na kutoa ajira kwa vijana wenzao.

Walikuwa ni miongoni mwa vijana waliokuwa na hamasa kubwa ya kujiajiri ili kujipatia kipato cha kue­ndesha familia zao pamoja na kutoa ajira kwa vijana wenzao.

Hata hivyo, changamoto ilikuwa jinsi ya kukuza mtaji wao ili kuanzisha kiwanda kidogo cha kutengeneza mapambo ya ndani kwa kutu­mia unga wa Gypsum.

Willson John Katibu wa Kikundi cha Umoja ni Nguvu Hondogo-Delini Kata ya Kib­amba anakiri wao ni wanu­faika wakubwa wa mikopo inayotolewa na Manispaa ya Ubungo.

Mikopo hiyo inatolewa chini ya kifungu cha 37A cha Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, sura 290 na kanuni za utoaji na usimamizi wa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu za mwaka 2019.

Kupata mikopo hiyo ina­hitajika wanawake na vijana waunde kikundi cha watu wasiopungua watano huku watu wenye ulemavu waki­takiwa kuwa wanakikundi wasiopungua wawili.

Wanufaika wa mikopo Manispaa ya Ubungo wakifuatilia mafunzo kabla ya kukabidhiwa mikopo.

Kikundi hicho kinataki­wa kiwe kimesajiliwa, kina akaunti ya benki yenye jina la kikundi na kijishughulishe na ujasiriamali au kiwe na kusudi la kuanzisha shughuli za ujasiriamali mdogo au wa kati.

John anasema Kikundi cha Umoja ni Nguvu kilianza mwaka 2020 kwa kuanzisha kiwanda kidogo cha kuten­geneza mapambo ya ndani kwa kutumia unga wa Gyp­sum.

Anasema kikundi kilianza na vijana 10 na sasa kina vijana wanane ambapo wa wanaume ni sita na wan­awake wawii wanaoendelea na mradi. Kikundi kilisajili­wa rasmi na Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo mwaka 2020 kwa cheti namba UMC/ VK/5174/2020.

Kikundi hicho kilianza shu­ghuli zake na mtaji wa Sh3.45 milioni ikiwa ni michango ya wanachama (kiingilio na ada) na msaada kutoka kwa wadau wa maendeleo. Fedha hizo zilitumika kujen­ga banda dogo la kufanyia kazi, kununua mashine tano za mikanda, vitendea kazi vingine na gharama za uen­deshaji. Mwaka 2021 wali­fanikiwa kupata mkopo wa Sh37.5 milioni kutoka Hal­mashauri ya Manispaa ya Ubungo.

“Februari 2021/2022 kikundi kilikidhi vigezo baa­da ya kutuma maombi ya mkopo Halmashauri na hivyo kufanikiwa kukopeshwa Sh37.5 milioni. Mkopo huu una kipindi cha marejesho cha miaka mitatu,” anasema John.

Kuhusu urejeshaji wa fed­ha hizo anasema mwanzoni walitia mkazo kuhakikisha fedha hizo wanazirudisha ili kupata mkopo mwingine.

“Baada ya kipindi cha miezi 3 walianza kureje­sha Mei 2022. Kufikia Julai 2022 kikundi kilikuwa kime­sharejesha jumla ya Sh3.12 milioni ambayo ni sawa na Sh 1.04 milioni kwa kila mwezi,” anasema John.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Patrobas Katambi (kulia) akimsikiliza mwakilishi wa kikundi cha vijana cha Umoja ni Nguvu alipotembelea baadhi ya vikundi vya vijana vya Manispaa ya Ubungo ambavyo vimenufaika na mikopo ya asilimia 10 wakati wa maadhimisho ya siku ya vijana duniani, 2022.

Anasema fedha walizope­wa zimewasaidia kuten­geneza karakana bora zaidi ya lle ya awali, kuongeza mashine 39 za kutengeneza mapambo aina tofauti na zile 5 za mwanzo, kuongeza mtaji kwa kununua mifuko 400 ya Gypsum Powder na mifuko 10 ya nyuzi (Fibers) na kununua vifaa vingine muhimu vya kazi kama mapipa, meza na rola za kufungashia.

Takwimu za Wizara ya Ofi­si ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) zilizotolewa na Waziri Ummy Mwalimu wakati akiwasili­sha bajeti yake ya 2021/22 bungeni zilionyesha kuwa Serikali imetenga Sh64.5 bilioni kwa ajili ya mikopo kwa vikundi 18,244 vya wan­awake, vijana na watu wenye ulemavu.

Kati ya fedha hizo, Sh25.8 bilioni zilitengwa kwa ajili ya vikundi 8,223 vya wanawake, Sh25.8 bilioni kwa ajili ya vikundi 6,966 vya vijana na Sh12.9 bilioni kwa ajili ya vikundi 3,055 vya watu wenye ulemavu.

Mikopo hiyo ni sehemu ya asilimia 10 ya mapato inayo­tengwa na kila Halmashauri ya Tanzania Bara kwa ajili ya vijana ambao hupata (asilim­ia nne), wanawake (asilimia nne) na watu wenye ulemavu (asilimia mbili).

John anasema mpaka sasa kikundi hicho kimefanikiwa kutengeneza ajira kwa vijana sita mbali ya wanakikundi, wawili kwa ajili ufungashaji na wanne kwa ajili ya kufyat­ua mikanda kwa lengo la kuongeza nguvu za uzalish­aji kutokana na wanakikundi kuwa wachache.

Kimeongeza uzalishaji kutoka mikanda 900 kwa wiki hadi 5400 kwa wiki, kuongeza bidhaa mpya za maua, kona (Angle) na Stick na kimeweza kulipa kodi ya shilingi laki sita (600,000) kwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ndani ya kip­indi cha miezi mitano baada ya kupata mkopo.

John anasema matarajio yao kwa sasa ni kuwa na kiwanda kikubwa kitakacho­zalisha bidhaa bora za kuto­sha kuhudumia soko la ndani na la nje ya nchi, kukuza ajira na kuinua uchumi wa vijana kwa kuwapa ajira na elimu ya ufundi, kumiliki eneo binafsi la kikundi badala ya eneo la sasa la kukodi, kurudisha mkopo kwa wakati ikiweze­kana kabla ya muda wa miaka 3 ili wengine nao wapate na kuanzisha uzalishaji wa gypsum board.

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Kheri James (katikati) akikabidhi mfano wa hundi ya Sh1.1 bilioni kwa vikundi vya wajasiriamali vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ikiwa ni utekelezaji wa sera ya uwezeshaji wananchi kiuchumi kwa kutenga asilimia 10 za mapato ya ndani.

“Tunamshuru Mungu kwa kutupa maono ya kuanzisha kiwanda hiki. Aidha tunashu­kuru Serikali ya awamu ya sita ya Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na Manispaa ya Ubungo kwa kutenga baje­ti hizi za kuwezesha vijana,” anahitimisha John.

Wakati wa maadhimisho ya wiki ya vijana duniani mwaka huu, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye ulemavu, Patrobas Katambi alitembelea baadhi ya vikun­di vya vijana vya Manispaa ya Ubungo ambavyo vimenufai­ka na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa na halmashauri kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu na kue­leza kuwa dhima ya Serikali ni kuona vijana wanajiajiri kwenye shughuli za uzal­ishaji wakisaidiwa na Hal­mashauri kwa kuongezewa mikopo isiyo na riba kama sheria inavyoelekeza.

Kwenye ziara hiyo Naibu­Waziri Katambi alitembelea kikundi cha Umoja ni Nguvu kinachojihusisha na uten­genezaji wa mapambo ya ndani kwa kutumia unga wa gypsum na kikundi cha Bria­co kinachojishughulisha na uzalishaji wa Kripsi za viazi mbatata na kuwataka vijana kuwa na malengo, kusudio na shabaha katika mipango kazi yao ili waweze kuzali­sha bidhaa zenye ushindani kwenye soko la ndani na nje.

Mweka Hazina wa kikundi cha watu wenye ulemavu cha Kibamba (Kibamba Disable Group), Stella Kalinga anas­ema kikundi hicho kilicho­anza mwaka 2021 kilikuwa na wanachama wanne ambapo baadaye mmoja alijitoa na sasa wamebaki watatu.

Anasema kikundi hicho kinajihusisha na mradi wa usafirishaji abiria kwa kutu­mia bajaji ambao ulitokana na mkopo waliyopata mwaka uliopita kutoka Halmashauri ya Ubungo.

“Baada ya kuunda kikundi chetu na kukisajili, tulienda Manispaa na Mungu akasaid­ia tukapata mkopo wa Sh8.5 milioni ambao tulikubaliana tuanzishe biashara ya bajaji. Tulitumia kiasi cha Sh7.3 mil­ioni kwa ajili ya kununulia bajaji na pesa kidogo iliyo­baki tulitumia kugharamia mahitaji mengine ili chombo hicho kiweze kufanya kazi,”anasema Stella.

Anasema bajaji hiyo wamemkabidhi mtu kwa ajili ya kufanya nayo biashara ambapo anawaletea fedha inayowasaidia kurejesha mkopo huo pamoja na kuki­dhi mahitaji ya familia zao.

“Mpaka sasa tumefaniki­wa kurejesha Sh 7.1 milioni na kiasi kilichobaki tunata­rajia kumalizia mwezi huu. Marejesho haya yametokana na fedha tunayoipata kutoka kwenye bajaji hiyo ambayo kiukweli imetusaidia kuki­dhi baadhi ya mahitaji yetu,” anasema Stella.

Anasema wakifanikiwa kumaliza mkopo huu wana­tarajia kuchukua mwingine ambao utawawezesha kila mtu kwenye kikundi hicho kuwa na bajaji yake.

Mwenyekiti wa kikundi cha kina mama cha Newton kilichopo Kimara Kilungule, Albina John anasema kikundi hicho kilianza mwaka 2019 kikiwa na wanachama 25 lakini sasa wapo 12 kutokana na wengine kushindwa kufuata matakwa ya mkataba walio­wekeana.

Albina anasema kikundi hicho kinajihusisha na shu­ghuli mbalimbali ikiwemo; kutenegeneza chaki, batiki, kufungasha asali mbichi, kusindika pilipili, kutenege­za siagi ya karanga, kute­ngeneza sabuni za maji na kutengeneza jiki.

 Kikundi cha kina mama cha Timasu ambao ni wanufaika wa mikopo ya Manispaa ya Ubungo wakiwa kwenye maonyesho ya ujasiriamali jijini Dodoma.

“Ili kupanua mtaji wa kikundi chetu Machi, 2021 tulipeleka maombi ya mkopo Halmashauri ya Ubungo na kwa bahati nzuri tulifani­kiwa ambapo halmashauri hiyo ilitupatia kiasi cha Sh50 milioni fedha ambayo ime­tusaidia kwa kiasi kikubwa kukuza biashara yetu kwa kununua vitendea kazi ikiwe­mo mashine mpya na kupata eneo la kudumu kwa ajili ya biashara,” anasema Albina.

“Kabla ya kupata mkopo huo tulikuwa na mashine moja tu ya kuzalisha chaki ambayo ilikuwa na uwezo wa kuzalisha kilo 800 za chaki kwa siku lakini baa­da ya kupata mkopo huo tuliongeza mashine tatu na sasa tunazo nne,” anasema Albina.

Albina anasema lengo la kikundi cha Newton ni kutengeneza ajira kwa wakina mama wengine kwa sababu wanafahamu kwamba chan­gamoto ya ajira ni kubwa.

Licha ya malalamiko ya baadhi ya wanawake na vijana kupewa kiasi kidogo cha fedha, Halmshauri ya Manispaa ya Ubungo ime­sema mikopo hiyo hutolewa kulingana na fedha uhitaji wa mradi ulioombewa baada ya upembuzi wa kina.

Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo imekuwa moja ya halmashauri vinara katika eneo hili ambapo kupitia mapato yake ya ndani ime­wawezesha wananchi katika makundi ya wanufaika kujik­wamua kiuchumi pamoja na kuchangia juhudi za kukuza uchumi.

Halmashauri hiyo imeku­wa ikitenga asilimia 10 ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya mfuko wa kuweze­sha vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulema­vu kila mwaka.

Toka Halmashauri ili­poanza kutekeleza agizo la Serikali la kutoa mikopo ya asilimia 10 kupitia mfuko wa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu mwa­ka 2017/2018, hadi kufikia April, 2021/2022 jumla ya Sh7.559 bilioni zimetolewa kwa vikundi 1350 vyenye wanufaika 10,163.

Mkurugenzi wa Hal­mashauri ya Ubungo, Bea­trice Dominic anasema kila mwananchi mwenye sifa ya kupata mikopo hiyo anakari­bishwa kupeleka maombi bila kujali itikadi ya chama chake wala kabila.

“Serikali iliweka fedha hizi ili kuhakikisha mjasiri­mali anakuza kipato chake na Taifa kwa ujumla, hivyo kwa yeyote anayetaka kupata mkopo huo hana budi kuom­ba ili aweze kuongeza kipato cha familia,” anasema Mku­rugenzi huyo.

Afisa Maendeleo wa Mani­spaa ya Ubungo anasema katika utoaji wa mikopo hiyo huzingatia zaidi andiko la mradi, uhalisia wa utekelez­aji wake kutoka kwa wanaki­kundi.

Anasema wanazingatia sheria ya utoaji wa mikopo hiyo na si vinginevyo ikiwe­mo kuwapatia watu mikopo walio kwenye vikundi bila kujali itikadi zao za vyama.

Anasema mikopo iki­tolewa, wana utaratibu wa kuwafuatilia wahusika kupi­tia maafisa wa maendeleo ya jamii katika kata ili kujua kama miradi iliyoombewa fed­ha ipo na inajiendesha.

“Hatua tunazochukua kwa vikundi ambavyo havi­jarejesha mikopo ni kuwa­fuatilia kujua changamoto na namna ya kukabiliana nazo ili waendeleze mradi na kufanya marejesho,” anas­ema Afisa Maendeleo huyo.

Hata hivyo, anasema mchakato wa kushughulikia changamoto mbalimbali ambazo zimejitokeza ikiwe­mo uchepushaji wa matumizi ya mikopo hiyo unafanyika.

Kuhusu utoaji wa elimu kwa vikundi hivyo Afisa Maendeleo anasema katika robo ya nne ya mwaka wa fedha 2021/2022, Idara ya Maendeleo ya Jamii ya Mani­spaa hiyo kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo kabla ya kutoa mikopo hutoa elimu na mafunzo ya kuwa­jengea uwezo kwa vikundi vinavyoomba kupatiwa mikopo pamoja na vikundi vingine katika Kata na Mitaa ya Halmashauri.

“Mafunzo yanayotolewa yanalenga kuwajengea uwezo kwenye uongozi, tabia za fedha, uendeshaji wa miradi, usimamizi wa fedha, uwekaji wa akiba, utunzaji wa kumbukumbu, matumizi ya nembo za ubora, vifun­gashio na marejesho yali­yotolewa kwa vikundi 1350 vilivyopatiwa mikopo,” ame­sema.

Kikundi cha kina mama cha Newton ambao ni wanufaika wa mikopo ya Manispaa ya Ubungo wakiwa kwenye maonyesho ya ujasiriamali jijini Dodoma.

Kwa sasa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo ina­sajili vikundi vinavyotege­mea kupata mikopo kupitia mfumo wa mtandao ulioele­kezwa na Serikali.

Ili kufanikisha usajili huo, vikundi vinapaswa kufika ofi­si za Kata na kupata maele­kezo ya usajili kwa Ofisa Maendeleo ya Jamii wa Kata au kutembelea Youtube kwa kuandika Ubungo Manispaa namna ya kusajili vikundi mtandaoni.

Makala hii imelipiwa na Manispaa ya Ubungo. Mwananchi Communications Limited (MCL) haihusiki kwa namna yoyote na bidhaa ama huduma zinazotangazwa humo na haitawajibika kwa chochote kitakachojiri ukiamua kuzitumia.