IMELIPIWA: FIBA watembelea Premier Project, wafurahishwa na uwekezaji uliofanyika
Muktasari:
Tanzania ni miongoni mwa mataifa ambayo yanajipambanua kufanya vizuri kwenye mpira wa kikapu japokuwa mwamko wake sio mkubwa ukilinganisha na mpira wa miguu.
Tanzania ni miongoni mwa mataifa ambayo yanajipambanua kufanya vizuri kwenye mpira wa kikapu japokuwa mwamko wake sio mkubwa ukilinganisha na mpira wa miguu.
Hili limesababisha wadau mbalimbali kuweka jitihada za kuhakikisha mchezo huo unakua na kutoa faida katika jamii ikiwemo ajira na kuiingizia Serikali mapato.
Premier Project iliyopo Kigamboni ni miongoni mwa juhudi kubwa zinazofanywa na wadau wa michezo nchini kuhakikisha kikapu kinapiga hatua na kuleta faida kwa Taifa.
Premier Project ni mradi unaohusisha miundombinu ya mpira wa kikapu unaotekelezwa katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam ambapo unahusisha akademi ya watoto wanaofundishwa kuhusu mchezo huo na unafadhiliwa na kampuni ya michezo ya kubashiri ya Premier Bet Tanzania.
Oktoba 25, 2022 ujumbe wa Shirikisho la Mpira wa Kikapu Duniani (FIBA) ulifanya ziara kwenye mradi huo na kuvutiwa na uwekezaji mkubwa uliofanyika.
Akizungumzia kuhusu Premier Project, Kamishna wa FIBA, Zulfikar Karim anasema ni mradi mzuri na ni jambo la kuungwa mkono kwani mchezo huo unahitaji nguvu za wadau katika uwekezaji.
“Mpira wa kikapu unahitaji uwekezaji mkubwa kutokana na miundombinu yake, hivyo ni lazima wadau wajitokeze kuwekeza kama ilivyofanyika kwenye mradi huu. Nawapongeza wadau hawa kwa juhudi hizi na nina uhakika mradi huu unakwenda kuleta mapinduzi makubwa kwenye mpira wa kikapu Tanzania,” anasema Karim.
Anasema Tanzania bado mwamko wa mpira wa kikapu uko chini ukilinganisha na mpira wa miguu lakini mwelekeo kwa sasa ni mzuri kutokana na jitihada za wadau katika kuwekeza kama ilivyofanyika kwenye Premier Project.
“Tanzania inahitaji sana uwekezaji kama huu kwa sababu mpira wa kikapu unahitaji miundombinu ya kuchezea iliyo bora tofauti na mpira wa miguu ambao mnaweza kuamua kuweka magoli tu, mkatafuta mpira mkacheza lakini huku ni tofauti,” anasema Karim.
Anasema FIBA wanatoa pongezi kubwa kwa uwekezaji uliofanyika na wao kama msimamizi mkuu wa mchezo huo wako tayari kuunga mkono juhudi hizo ili kuhakikisha wanaleta mapinduzi kwenye mpira wa kikapu Tanzania.
Mbali na ujumbe wa FIBA, ziara hiyo pia ilihusisha maofisa wa Chama cha Mpira wa Kikapu Tanzania (TBF), Chama cha Mpira wa Kikapu Dar es Salaaam (BD) pamoja na nahodha wa Timu ya Taifa ya Mpira wa Kikapu ya Tanzania, Omary Mohammed.
Wakizungumza na gazeti hili baadhi ya watoto kwenye akademi hiyo walishukuru kuletewa mradi huo kwani utawasaidia kutimiza ndoto zao za kuwa wachezaji wakubwa wa mpira wa kikapu.
Briton Michael anasema kitu kilichomvutia kuingia kwenye akademi hiyo ni mapenzi yake kwenye mpira wa kikapu na anaamini kwamba kupitia Premier Project ataweza kufanikisha ndoto zake za kuwa mchezaji mkubwa nchini.
“Nilivyokuwa naona jinsi mchezo huu unavyochezwa nilipenda sana jinsi wanavyodunda mpira na kuruka juu. Nikamwambia mama nataka nicheze, akaniruhusu lakini sikuwa na sehemu ya kuchezea. Ulivyokuja mradi huu umenisaidia kwani hapa tunafundishwa vitu vingi ambavyo vimenifanya kuupenda zaidi,” anasema Briton.
Ramadhani Ayubu anasema amefurahia mradi huo kwani unawasaidia kufanya mazoezi na kuweka miili yao vizuri, pia unawapa mbinu za mpira wa kikapu ambao anaupenda sana.
“Akademi hii imenisaidia kufanya mazoezi na kuboresha afya yangu lakini pia kocha wetu anatusaidia kutupa mbinu mbalimbali za kucheza mpira wa kikapu jambo ambalo limenifanya niendelee kuupenda mchezo huu. Nawashauri watoto wengine kuja kushiriki kwani kila mtoto anaruhusiwa kuja hapa,” anasema Ramadhani.
Michael Mako anasema anapenda kucheza mpira wa kikapu lakini alikuwa anakosa nafasi ya kuchezo kwa sababu shuleni kwao kila mtu anapenda mpira wa miguu hivyo alivyosikia akademi hiyo inaanzishwa alifurahi.
Michael alishukuru kwa kuletewa akademi hiyo kwani itawasaidia kutimiza ndoto zao za kucheza mpira wa kikapu na kuwataka watoto wengine wanaopenda mchezo huo kujiunga kwenye akademi hiyo.
Mkurugenzi wa mradi huo, William Mziray anasema lengo la mradi huo ni kuhakikisha wananyanyua mpira wa kikapu nchini.
“Tumeamua kuanzisha mradi huu ili kuinua mpira wa kikapu Tanzania kwa sababu mchezo huu ni miongoni mwa michezo inayokua kwa kasi duniani na wenye pesa nyingi hivyo tunataka na sisi kama Taifa kuweka mazingira mazuri ya kuukuza,” anasema Mziray.
Anasema ili kuweza kuendeleza mchezo huo wameamua kuwekeza kwa watoto kwa kuamini kwamba kundi hilo likipatiwa mafunzo na miundombinu bora litasaidia Taifa kuwa na kizazi bora cha mchezo huo.