Kifahamu kilimo cha kisasa cha maharage-2

Muktasari:
Kiasi cha mbegu
Ili kupanda ekari moja unahitaji kuwa na kiasi cha kilo 30 mpaka 40 za maharage. Hii ni sawasawa na kilo 80 hadi 90 za maharage kwa hekta.
Makala ya wiki iliyopita iliishia katika kipengele kuhusu maandalizi ya mbegu. Endelea.
Kiasi cha mbegu
Ili kupanda ekari moja unahitaji kuwa na kiasi cha kilo 30 mpaka 40 za maharage. Hii ni sawasawa na kilo 80 hadi 90 za maharage kwa hekta.
Unaweza kupanda mbegu moja au mbili katika kila shimo, lakini mbegu mbili ni bora zaidi na huleta mavuno mengi kwa eneo.
Nafasi ya upandaji
Ikiwa utapanda mbegu mbili za maharage katika kila shimo tumia nafasi ya sm 50 kwa sm 20 yaani sm 50 kati ya mstari na mstari na sm 20 kati ya mmea na mmea (shimo na shimo).
Ukipanda mbegu moja katika kila shimo, tumia nafasi ya sm 50 kwa sm 10. Hii ikuletee mimea kati ya 150, 000 na 200, 000 katika hekta moja.
Kudhibiti magugu
Maharage yanahitaji palizi mbili za jembe la mkono. Katika palizi ya kwanza, ondoa magugu shambani mara tu yanapoonekana, lakini hili lifanyike angalau wiki ya pili tangu maharage kuota.
Palilia tena kabla maharage hayajachanua. Kupalilia maharage yanayochanua au yenye matunda, kunasababisha kupukutisha maua au matunda.
Lakini pia unaweza kutumia madawa ya kuuwa magugu kama vile Galex 500EC, Stomp 500EC, Dual gold, sateca.
Mahitaji ya mbolea
Maharage hayahitaji naitrojeni kwa wingi kwa sababu mizizi ya maharage husaidiana na viumbe hai (nitrogen fixing bacteria) waishio kwenye udongo kutengeneza nitrogen.
Hata hivyo maharage yanahitaji madini ya fosforasi kwa ajili ya kuboresha mizizi na potashi kwa ajili ya kuuandaa mmea kwa ajili ya kutoa maua mengi na kuzaa matunda bora.
Ikiwa shamba lililimwa zao ambalo liliwekwa mbolea kama vile Urea au CAN, basi huna haja ya kuweka tena mbolea za naitrojeni, badala yake unaweza kuweka TSP au DAP Kg 60 kwa hekta wakati wa kupanda. Au mbolea ya minjingu (Minjingu Rock Phosphate) Kg 250 kwa hekta moja wakati wa kupanda.
Kama shamba limechoka sana au halikuwekwa mbolea za naitrojeni msimu uliopita, tumia NPK katika uwiano wa 5:10:10 kiasi cha Kg 30 kwa hekta; nayo iwekwe wakati wa kupanda.
Mbolea zote ziwekwe sentimita tano hadi 10 kutoka kwenye shina/shimo la mmea na urefu wa sentimita 3 hadi 5 kwenda chini. Pia unaweza kutumia mbolea samadi (tani 5 - 10 kwa hekta) au mbolea ya kijani (green manure, tani 5 kwa hekta).
Mwaga/tawanya samadi kwenye shamba lote halafu ichangane vizuri na udongo kwa kulima kwa plau la trekta au ng’ombe). Maana yake ni kwamba mwaga samadi kabla ya kulima shamba lako kwa trekta au ng’ombe.
Mbolea ya kijani inapatikana kwa kusafisha shamba halafu ukaliacha mpaka majani/magugu yakaota kisha ukalilima kwa trekta au ng’ombe likiwa na magugu hivyo hivyo, lakini kabla hayajatoa mbegu halafu ukapanda. Mbolea ya minjingu inaweza kutumika pamoja na samadi na mbolea ya kijani.
Maharage huhitaji mvua ya kutosha kipindi cha kabla ya uwekaji maua na kipindi cha ukuaji wa vitumba vya maharage (podding).
Makala haya yameandaliwa na Mogriculture Tz, inayotoa mafunzo ya kilimo bora na ufugaji wa kuku. www.mogriculture.com. 0655570084