|
Papic kujifunga Yanga hadi 2011 |
Send to a friend |
|
Monday, 26 April 2010 21:04 |
|
Imani Makongoro
KOCHA Mserbia, Kostadin “Bill Clinton” Papic amebadilisha uamuzi wake wa kuikacha Yanga baada ya kukubali kusaini mkataba mwingine wa mwaka moja na klabu hiyo ya mtaa wa Jangwani na Twiga.
Kwa mujibu wa taarifa ilizozipata Mwananchi jana zinasema kwamba kocha Papic amekubali kusaini mkataba wa mwaka moja utakaoanza mwezi ujao ikiwa ni wiki moja tangu alipotangaza kuikacha klabu hiyo kwa kushindwa kumlipa mshahara.
Papic alichukua uamuzi huo baada ya kukutana na viongozi wa klabu hiyo kujadili kwa undani kuhusu malipo yake.
Kiongozi mmoja wa Yanga, alisema Papic alikutana na mfadhili Yusuf Manji na kukubalina kuyamaliza matatizo yake yote yaliyojitokeza kwenye mkataba wake wa kwanza.
Moja ya matatizo ni madai yake ya mshahara na malalamiko yake ya kutoheshimwa. Tangu alipokataa kuongeza mkataba wake mwaka jana mwezi Oktoba.
Mserbia huyo anategemea kusaini mkataba mpya mapema wiki ijayo utakaodumu hadi Mei 2011, kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari.
Alipoulizwa Papic kuhusu suala hilo alisema kwa kujiamini kwamba watasaini mkataba mpya na klabu hiyo na amebadilisha uamuzi wake wa kuikacha timu hiyo.
“Viongozi pamoja na mfadhili wamekubaliana kuyamaliza matatizo yangu yote yaliyokwamisha utendaji wangu wa kazi, kwa sasa tumekubaliana kusaini mkataba mpya na kubadili uamuzi wangu,” alisema Papic.
Alisema kwa sasa ameweka mawazo yake katika kutengeza timu yake kwa kufanya usajili imara kwa ajili ya msimu ujao.
“Bado hatujavunja kambi, tuna wachezaji wapya kadhaa waliokuja kufanya majaribio, lengo letu ni kumaliza majaribio na wachezaji wote wakiwepo kabla ya kuwapa likizo,” alisema.
Katibu mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako alithibisha taarifa hiyo kwa kusema klabu hiyo sasa wanajiandaa kwa kusaini mkataba huo mpya.
Mwalusako alisema pande zote mbili zimefikia makubaliano na sasa mawazo yote ni katika kutengeza kikosi bora kwa msimu ujao wa ligi.
“Ni kweli tumeandaa mkataba mpya kwa ajili ya kocha, aliomba tuujadiri mkataba wake na tumefikiria makubaliano,” alisema Mwalusako.
Alisema Papic ametaka mkataba wa mwaka moja utakaoendana sambamba na Ligi Kuu ya Vodacom msimu ujao.
Wakati huo huo, Mwalusako amesema kitendo cha kocha wao, Papic kuonyesha dalili za kuishangilia Simba katika mchezo dhidi ya Haras el-Hodood hakumaanishi kuwa amekimbia kwenye klabu hiyo.
Wakati Papic akifanya hivyo na kukabidhiwa fulana na skafu nyekundu na mashabiki wa Simba, upande wa majukwaa ya Yanga walikuwa wametulia wakishangaa kinachoendelea cha kocha wao huku wengine wakijiulizwa maswali bila kupata majibu.
Ni wazi mashabiki walikuwa wakiunganisha hilo na mahojiano maalum ya kocha huyo na gazeti dada la Michezo la Mwanaspoti la mwishoni mwa wiki lililochapisha habari kuwa kocha huyo amebwaga manyanga kufundisha Yanga.
Kocha huyo alikuwa akilalamikia kutolipwa fedha zake za mshahara ambao mfadhili wa klabu hiyo, Yusuf Manji ndiye anayemlipa. Papic alikaririwa akisema amechoka kusotea mshahara wake na anaondoka Yanga na wala hakufukuzwa.
Mwalusako alisema kuwa Papic ni mwanamichezo na anapenda soka ndiyo maana hakuona tatizo kwenda kuwaunga mkono Simba. "Unajua hata sisi tumeiona, mwenyewe nilikuwepo uwanjani pale , nikaona na niliongea naye lakini akaniambia ni kutia hamasa tu," alisema Mwalusako.
Juu ya fedha zake za mshahara, Mwalusako alikiri uongozi kumwandikia barua mfadhili wao kutaka ufahamu juu ya hali hiyo inayojitokeza, lakini akasema zaidi yatapenyezwa katika kikao cha Kamati ya Utendaji ya klabu .
|
Comments