Wadakwa na meno ya tembo

Muktasari:

  • Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa,  George Kyando amesema  leo meno hayo yalifungwa kwenye  viroba yakiwa yamechanganywa na miwa kwa kigezo kuwa wamebeba mbegu za miwa ili wasikamatwe na kuupakia` kwenye pikipiki.

Sumbawanga.  Jeshi la Polisi Mkoani Rukwa  linawashikilia watu wanne  wakazi wa kijiji cha Mkangale wilayani Nkasi, kwa tuhuma ya kukamatwa na meno ya tembo yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 67.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa,  George Kyando amesema  leo meno hayo yalifungwa kwenye  viroba yakiwa yamechanganywa na miwa kwa kigezo kuwa wamebeba mbegu za miwa ili wasikamatwe na kuupakia` kwenye pikipiki.

Amesema kwamba watuhumiwa hao wamekamatwa jana mchana kufuatia msako uliofanywa na  polisi katika pori la Akiba la Lwafi lililopo wilayani humo kwa kushirikiana na askari wa wanyama pori.

Amesema  watuhumiwa walikuwa wakisafirisha meno hayo kutoka kijiji cha Mkangale kwenda Wampembe kwa lengo la kutafuta soko la bidhaa hiyo haramu.

Akiwataja majina watuhumiwa hao Evans Tenganamba ,Elisha John , Sandu John  na Justin Kapembwa.

Kamanda wa Kyando ametoa wito kwa wananchi kuachana na tabia ya uwindaji haramu kwani ni kosa la jinai kwa yeyote atakayebainika kuwa anajihusisha na uwindaji huo haramu polisi pamoja na uongozi wa wanyamapori hawatawafumbia macho na lazima sheria ifuate mkondo wake.