Lissu, Nchemba, Zitto waguswa na msiba Arusha

Dar es Salaam. Baadhi ya wanasiasa nchini wametuma salamu za rambirambi kwa wanafamilia, ndugu, jamaa na marafiki katika mitandao mbalimbali ya kijamii kutokana na ajali iliyotokea Arusha na kugharimu maisha ya wanafunzi, walimu na dereva.

Katika akaunti yake ya Twitter, Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lissu ameandika, “Nimesikitishwa na vifo zaidi ya 31 vilivyosababishwa na ajali mbaya iliyotokea Karatu. Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema.”

Waziri wa Mambo ya Ndani Mwigulu Nchemba, ameandika katika ukaunti yake ya Twitter, “Natoa pole kwa familia, ndugu, jamaa na shule ya Lucky Vincent kwa msiba huu mzito uliopata Taifa letu uliotokana na ajali mbaya pale Karatu. Tumepoteza watoto wetu ambao wazazi wao, ndugu zao na Taifa kwa ujumla liliwategema. Kwa kuwa Mungu wetu anaishi na kumiliki tuendelee kuziombea familia zilizoguswa na msiba huu, watoto wetu wapumzike kwa amani.”

Naye Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe, “Moyo wangu umesinyaa baada ya kusikia taarifa za ajali ya watoto wetu huko Karatu. Natoa salamu zangu za rambirambi kwa wazazi wa wanafunzi wa shule ya St Lucky kwa ndugu na familia za walimu na wafanyakazi wa shule waliopoteza maisha.Huu ni msiba mkubwa sana. Huzuni haielezeki. Nawaombea kwa Mola awape wazazi na ndugu wote moyo wa subira katika mtihani huu. Ni msiba wa Taifa zima.”