Sheria ya matumizi ya ramani yaja

MUSWADA WA SHERIA YA SHIRIKA LA MAWASILIANO WATUA BUNGENI

Muktasari:

Mswada wa sheria hiyo utasaidia kudhibiti matumizi ya ramani potofu

Dodoma. Serikali imewasilisha muswada wa sheria ya marekebisho ya sheria mbalimbali wa mwaka 2017, ambapo moja ya marekebisho hayo ni kuweka faini ya hadi Sh10 milioni kwa atakayesambaza ramani potofu.

Akiwasilisha muswada huo bungeni mjini Dodoma leo Jumatano, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), George Masaju amesema adhabu kwa kosa hilo itakuwa faini isiyopungua Sh5 milioni lakini isiyozidi Sh10 milioni.

Endapo atashindwa kulipa faini hiyo, atalazimika kutumikia kifungo kisichopungua miezi sita lakini kisichozidi miaka miwili.

Masaju amesema lengo la marekebisho ya kifungu hicho kinachohusu upimaji na ramani ni kudhibiti ramani zinazopotosha mipaka sahihi ya maeneo.

Marekebisho hayo yana lengo la kumpatia mkurugenzi wa upimaji na ramani haki ya kipekee ya kuandaa, kutengeneza na kusambaza ramani zote zinazoonyesha mipaka ya mikoa na nchi.