Azam yatangaza kikosi cha kuivaa Triangle United, Ngoma, Chilunda waanzia nje

Muktasari:

Chirwa na Djodi wanacheza kwa kuelewana kutokana na Djodi kuwa na uwezo wa umiliki mpira kwa hali ya juu ambapo akisaidiana na Chirwa mwenye nguvu basi mabeki wa timu pinzani huwa wanapata tabu.

Dar es Salaam. Washambuliaji Donald Ngoma na Shaban Idd Chilunda wameanzia benchi wakati Azam FC ikishuka uwanjani kusaka ushindi dhidi ya Triangle United katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika leo saa 10:00 jioni kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi.

Katika mchezo huo kocha Ettiene Ndayiragije ameamua kuwaweka benchi Ngoma na Chilunda akiwaanzisha nyota wake Richard Djodi na Obrey Chirwa.

Tangu Ndayiragije atue Azam msimu huu Ngoma ameshindwa kupata namba katika kikosi cha kwanza cha mabingwa hao wa Kombe la FA.

Chirwa na Djodi wameonyesha maelewana mazuri tangu mchezo uliopita dhidi ya Fasil Kenema ambao Azam ilishinda nyumbani.

Katika eneo la kiungo Frank Domayo leo ataanza pamoja na Salum Abubakar wakiwa na jukumu la kuilinda ngome yao huku wakipitisha pasi za mwisho kwa washambuliaji wao.

Kikosi cha Azam: Razack Abarola, Nico Wadada, Bruce Kangwa, Daniel Amoah, Yakub Mohamed, Frank Domayo, Salum Abubakari, Idd Seleman ‘Nado’, Richard Djodi, Obrey Chirwa na Emmanuel Mvuyekure.

Wachezaji wa akiba Mwadini Ally, Mudathir Yahya, Idd Kipagwile, Donald Ngoma, Masoud Abdallah, Shaban Chilunda na Oscar Masai.